Sunday, April 12, 2015

Mtanzania Al-Shabaab

Wazazi wa Mtanzania Al-Shabaab

Na Fredy Azzah, Dar es Salaam
WAZAZI wa Mtanzania Rashid Charles Mberesero (21), anayetuhumiwa kuwa mmoja wa wanamgambo wa Al-Shabaab ambao walifanya mauaji katika Chuo Kikuu cha Garissa nchini Kenya na kuua wanafunzi 148, wamefunguka na kueleza siri ya mtoto wao huyo.
Wakizungumza na MTANZANIA kwa nyakati tofauti jana, walisema wakati kijana huyo akihusishwa na tukio hilo lililotokea Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo, walikuwa wakijua mtoto wao yupo shuleni mkoani Dodoma.
Akizungumza na MTANZANIA jijini Dar es Salaam jana, baba mzazi wa mtoto huyo, Charles Mberesero, alisema mwanawe huyo ni mwanafunzi wa kidato cha tano katika Shule ya Sekondari Bihawana iliyopo mjini Dodoma.
Alisema kwa muda mrefu mtoto wake alikuwa akilelewa na mama yake mzazi huko Gonja, Same mkoani Kilimanjaro, lakini kwa muda mfupi alioishi naye hakuwahi kufikiri kwamba angeweza kujihusisha na tukio kama hilo.
“Rashid alizaliwa mwaka 1994 huko Gonja Same, shule ya msingi aliyosoma siikumbuki, lakini sekondari najua kidato cha kwanza hadi cha nne alisoma katika Shule ya Gonja,” alisema.
Akimwelezea tabia yake, alisema Rashid ni kijana mtaratibu na mvumilivu sana.
“Alipokuwa akisoma O’ level nilikuwa nawasiliana naye sana, lakini kama mwaka mmoja na nusu uliopita tulikuwa hatuna mawasiliano ya karibu.
“Sasa hivi alikuwa anasoma PCB kwenye Sekondari ya Bihawana Dodoma. Kwenye matokeo ya kidato cha nne alipata daraja la pili na michepuo yote ya masomo ya Sayansi ilikubali, lakini akaamua kusoma PCB,” alisema na kuongeza.
“Juzi baada ya kutokea hayo yaliyotokea huko Kenya niliongea na mama yake, akaniambia mtoto alikuwa likizo ya kama wiki mbili na Machi 21, mwaka huu aliaga nyumbani kwamba anarudi shuleni Dodoma.
“Na unajua mambo ya huko kijijini baada ya mtoto kusema anasafiri kwenda Dodoma shuleni hakuna mtu aliyefuatilia hadi baadaye tulipokuja kusikia hayo ya Kenya.” Alisema kutokana na alivyoshtushwa na tukio hilo, tangu alivyopata taarifa zake siku ya Jumapili, alipata presha na jana ndipo aliweza kupata ahuweni na kutoka nyumbani.
UHUSIANO WAKE NA MWANAYE
Baba huyo alisema uhusiano wake na mtoto wake haukuwa mzuri sana kwa sababu alimtaka abadilishe dini yake akakataa.
“Nilikuwa namshawishi afuate dini yangu, mimi ni Mkatoliki kwa hiyo kuna wakati alikuja kwangu akakaa kama mwezi mmoja nikawa naenda naye kanisani, nikawa namshawishi abatizwe.
“Alikataa akasema anafuata dini ya mama yake… baada ya kuzaliwa sikumfuatilia sana kwa sababu mama yake aliolewa na mtu mwingine, sasa pale mimi kuzungumza naye kila saa isingewezekana,” alisema.
Alisema katika kipindi cha mwezi mmoja alioishi naye alikuwa akitembea naye muda mwingi, lakini asipokuwapo alikuwa anakaa ndani na pindi akitoka anakwenda msikitini.
SERIKALI ICHUNGUZE SHULE
Mberesero alisema kwa muda aliomjua mtoto wake huyo, anafahamu kwamba si mtu wa kutoka sana nyumbani kwa hiyo anashindwa kujua ni wapi alipojifunzia mambo ya kigaidi.
“Mimi kwa kweli naiomba tu Serikali ichunguze hizi shule ni nini hasa watoto wanafundishwa huko, kwa sababu leo imekuwa ya huyu anayesoma huko Dodoma, juzi hapa tumeona huyo wa Zanzibar.
“Hawa wote ni watoto wadogo, bila ushawishi mkubwa hawawezi kufanya hivi vitu. Mama yake huyu ni mlezi mzuri tu na ana watoto wengine, ni kwa nini tu huyu ndiyo aende huko? Ni lazima Serikali iangalie hili kwa makini,” alisema.
Akizungumza kwa masikitiko, alisema anaamini kwamba mtoto wake huyo alikuwa na akili sana darasani na endapo angeendelea na masomo yake angefika mbali.
“Sijui ameingiaje huku, angekuja kufika mbali sana,” alisema.
MAMA MZAZI ANENA
Akizungumza kwa njia ya simu na gazeti hili, mama mzazi wa Rashid, Fatma Ally, alisema mwaka jana mtoto wake huyo alifaulu mtihani wa kidato cha nne na kupangiwa kujiunga na kidato cha tano katika Shule ya Sekondari Kingwe iliyopo mkoani Dodoma.
Alisema alivyofika kwenye shule hiyo alibaini haikuwa na mchepuo wa Sayansi aliokuwa akisoma, hivyo akaomba kuhama na ndipo alipopata nafasi Shule ya Sekondari Bihawana.
“Kwenye shule aliyopangiwa alikaa kama miezi miwili akisubiri apate nafasi kwingine, shuleni huko alipelekwa na baba yake mlezi na mwezi wa tatu mwaka huu alirudi nyumbani akakaa kama wiki mbili.
“Hakusubiri likizo iishe, akasema kwa sababu sisi ni Waislamu haisubiri Pasaka, nikamwandalia vitu vyake akasema anaenda shuleni,” alisema.
Alisema siku ya Jumapili iliyopita akiwa sokoni, ndipo alipopata taarifa za mwanaye huyo kukamatwa nchini Kenya akihusishwa na ugaidi.
“Nilipigiwa simu na ndugu yangu mmoja akasema amesikia kwenye redio za Kenya kwamba kuna Mtanzania amekamatwa huko kwa ugaidi na ana jina kama la mtoto wangu.
“Baadaye tena baba yake akanipigia simu akinipa taarifa hizo, kwa kuwa Rashid alikuwa ametuaga anaenda shuleni ilibidi tuzungumze na ndugu zetu walioko Dodoma ili waende shuleni kwake pale wajue kama yupo shuleni.
“Walivyoenda huko wakamkosa na walimu wakawaambia kulikuwa na likizo kwa hiyo labda baada ya likizo ndiyo Rashid anaenda shuleni, nilivyosikia hivyo nikajua moja kwa moja kuwa yeye ndiye huyo aliyekamatwa huko Kenya,” alisema.
Mama huy, alisema hali hiyo ilimshangaza na kumpa wakati mgumu kwani anajua kuwa tangu mwanaye huyo azaliwe, hajawahi kutoka nje ya nchi na hata huko Kenya hapafahamu.
“Hata akiwa nyumbani akitoka sana anaenda msikitini, sijui huo ushawishi kaupata msikitini ama huko shuleni,” alisema.
Alisema siku mwanaye huyo anaenda shule, alimpa Sh 90,000 kwa ajili ya nauli na matumizi mengine.
“Hata akiwa shuleni akiniambia ana shida huwa namtumia fedha yoyote niliyonayo, naweza kumtumia Sh 5,000, 10,000 ama 20,000,” alisema.
Gazeti hili lilipotaka kujua kama mama huyo ana mpango wa kwenda Kenya kumwona mtoto wake huyo, alisema hadi sasa haelewi nini cha kufanya.
“Mimi ni mwanamke sijui huko naendaje kwani ile ni nchi ya watu, sijui utaratibu wa kwenda na hata nikienda sijui kama nitaruhusiwa kumwona,” alisema.
UONGOZI WA SHULE
Wakati hayo yakiendelea, waandishi wetu Debora Sanja na Ramadhan Hassan wa mkoani Dodoma wanaeleza kuwa Mkuu wa Shule ya Sekondari Bihawana, Mbilinyi Joseph, alithibitisha kwamba Rashid Charles Mberesero ni mwanafunzi wa shule hiyo.
Akizungumza na MTANZANIA jana nyumbani kwake, Mbilinyi alisema tangu mwanafunzi huyo alipoondoka wakati wa likizo Novemba 25, mwaka jana hadi sasa hajarejea shuleni.
“Kwa kweli alikuwa ni mwanafunzi wa kawaida, mimi nilikuwa simjui ila kuna siku mimi alinishangaza sana hali iliyonisababisha kumpa adhabu,” alisema.
Alisema siku hiyo akiwa maeneo ya shule majira ya jioni alimkuta kavaa kofia za Waislamu maarufu kama balaghashia, akamwamuru avue na aichane kwa kuwa hakuwa msikitini na shule hiyo ni ya mchanganyiko wa Waislamu na Wakristo.
“Nilipomwamuru vile akasema hawezi kuivua wala kuichana kwa kuwa amezoea kuivaa, majibu hayo yalinipa hofu kweli nikamwambia kesho yake aje afisini asubuhi.
“Alipokuja ofisini nikamwamuru tena aivue kofia yake na aichane akaniambia hawezi kufanya hivyo kwa kuwa ni kinyume na sheria za dini ya Kiislamu.
“Nikamwambia namrudisha nyumbani akamlete mzazi wake akasema sawa, bado jibu hilo likanishtua pia kwa kuwa hakuonekana kushtuka na adhabu hiyo, nikamwambia aandike barua ya kujieleza akaandika na kudai yupo tayari kuacha shule kuliko kuivua na kuichana kofia ambayo yeye aliita balaghashia,” alisema.
Alisema kutokana na majibu yake akaamua kuwaita walimu wa dini ya Kiislamu wakazungumza nae akakubali kupewa adhabu, lakini cha kushangaza kuanzia siku hiyo hakuonekana tena shuleni.
“Siku aliyoondoka ilikuwa siku ya mtihani ambapo ulikuwa umebaki mtihani mmoja wamalize ili wafunge shule,” alisema.
Mkuu huyo wa shule alisema hawakuwa na jinsi ya kufanya zaidi ya kusubiri siku ya kufungua shule kuona kama atarejea, lakini hakurejea tena.
Alisema hata hivyo hawakuwa na wasiwasi sana walijua anaweza kurudi shule kwa kuwa baadhi ya wanafunzi huchelewe kuripoti shuleni kutokana na sababu mbalimbali.
“Lakini baada ya kupotea shuleni niliwaita tena viongozi wa dini ya Kiislamu ambao ni wanafunzi wenzake, nikawauliza kuhusu Rashid wakasema hata wao wanamshangaa kwa kitendo chake cha kuvaa kofia shuleni,” alisema.
Mkuu huyo wa shule alisema siku tatu baada ya kufunga shule kuna mwanafunzi wa kidato cha sita, Hassan Kissuda alimwomba ampigie simu ambapo alidai alikutana na Rashid Dodoma Mjini akidai anakwenda Kahama.
Alisema Rashid alichukua namba ya simu ya Kissuda akadai atampigia, lakini hakumpigia hadi leo.
“Shule ilipofunguliwa nikatafuta namba ya mzazi wa Rashid katika vitabu vya usajili vya shule nikapiga simu lakini haikupokewa.
“Baada ya kusikia jina la Rashid kwenye vyombo vya habari akihusishwa na tukio la ugaidi Kenya, Aprili 6 mwaka huu nikaipiga tena namba ile ile ikapokewa na baba yake ambaye kumuuliza akasema tukio hilo ni la kweli.
“Hata hivyo baba yake alisema jina la mtoto ni la kweli, lakini picha zinazoonyeshwa kwenye magazeti sio zake, lakini yaye baba yake alikwenda Polisi Makao Makuu akaonyeshwa picha hizo na kuthibitisha kwamba ni mwanaye,” alisema.
Akizungumzia maendeleo ya kitaaluma ya Rashid, alisema hawezi kuyasemea sana maendeleo yake kwa kuwa mwanafunzi huyo alihamia Agosti mwaka jana akitokea Shule ya Sekondari Kigwe.
Kwa mujibu wa matokeo yake ya muhula uliopita alikuwa na wastani wa C.
Alisema yeye kama mkuu wa shule ameshtushwa na tukio hilo kwa kitendo cha shule kukaa na mtu mwenye uwezo wa kuua wenzake na kwamba tukio hilo limechafua shule yao.
“Hili jambo linatisha sana, limeleta hofu kubwa, shule kuishi na Al Shaabab inatisha, ukimwona kijana mwenyewe alikuwa ‘very polite’, lakini hata hivyo yale majibu ya siku ile mimi yalinitisha sana, alikuwa ananijibu kwa upole, lakini majibu makavu,” alisema.
WANAFUNZI WENZAKE
MTANZANIA lilizungumza na wanafunzi wenzake wa kidato cha tano mchepuo wa PCB, ambapo mmoja wao, Lowassa Mayon alidai Rashid alikuwa mbinafsi na hakupenda kuzungumza na wenzake.
“Darasani alipenda kukaa mbele, alikuwa mpole sana na hakupenda kuzungumza na yeyote na ilikuwa ni vigumu mtu kumfuata na kuzungumza nae,” alisema.
AKIRI KUWA AL SHABAAB
Baadhi ya vyombo vya habari vya Kenya vimeripoti kuwa tayari Rashid amekiri kuwa yeye ni mwanachama wa Al Shabaab.
Juzi watu watano walifikishwa mahakamani jijini Nairobi, lakini Rashid ambaye ni mtuhumiwa wa sita, akuwepo mahakamani.
Vyombo vya habari vya nchi hiyo viliripoti kuwa Rashid anayetambulika sana kama Rehani Dida, hakuwa mahakamani kwa sababu alisafiri na maofisa wa uchunguzi kutafuta ushahidi zaidi baada ya kukiri kuwa yeye ni mfuasi wa Al-Shabaab.
Mwendesha mashtaka Daniel Karuri, aliiambia mahakama kuwa maofisa wa polisi wanafuatilia taarifa za kijasusi zinazohusisha washukiwa hao watano na shambulio la Alhamisi.
Waliofikishwa mahakamani ni Mohammud Adan Surrow ambaye ni mmiliki wa hoteli ambayo magaidi wanadaiwa kuishi kabla ya kutekeleza mauaji hayo.
Osman Abdi Dakane, mlinzi chuoni hapo aliyekamatwa baada ya kuonekana akijaribu kupiga picha waathiriwa wa shambulio hilo huku akiwa anawasiliana kwa simu na watu wasiojulikana.
Mohammed Abid Abikar, Hassan Adan Hassan na Sahal Diriye Hassan wanaodaiwa kuwaletea silaha magaidi, na walinaswa walipokuwa wakijaribu kutorokea nchini Somalia baada ya mauaji hayo.

Mtanzania
Read more



Habari Zinazoendana

2 days ago

Mtanzania

Siri mpya Mtanzania Al-Shabaab

David-MisimeNa Waandishi Wetu, Dar na Dodoma
SIRI mpya juu ya Mtanzania Rashid Charles Mberesero, anayehusishwa na tukio la kigaidi kwenye Chuo Kikuu cha Garisa nchini Kenya zimeibuka.
Kwa mujibu wa habari zilizoripotiwa jana na vyombo vya habari vya Kenya, Mtanzania huyo anayedaiwa kuwa miongoni mwa magaidi wa Al-Shabaab walioua watu 148 katika chuo hicho, endapo angesalimika baada ya tukio hilo, angepelekwa Somalia yalipo makao makuu ya kundi hilo la kigaidi.
Hayo yalibainishwa jana na mwendesha...

No comments:

Post a Comment