Tuesday, June 16, 2015

WASIRA KUDHAMINIWA IRINGA LEO.

WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasirra
amesema yupo tayari kumuunga mkono mgombea
yoyote atakayeteuliwa na Chama cha Mapinduzi (CCM)
kupeperusha bendera ya chama hicho katika
kinyang’anyiro cha urais Oktoba mwaka huu endapo
nafasi hiyo haitaangukia mikononi mwake.
Pamoja na ahadi hiyo, amesema hawezi kutoa jibu lolote
kwasasa kama atagombea tena au hatagombea ubunge
katika jimbo lake la Bunda kwasababu haijaingia katika
kinyang’anyiro hicho cha urais kwa ajili ya kushindwa.
Akizungumza na wanahabari kabla ya kukutana na
wadhamini wake zaidi ya 100 waliojitokeza kumdhamini
mjini Iringa jana, Wasira alisema; “ mimi ni mtu mwenye
uzoefu mkubwa wa kuongoza watanzania, kwahiyo nina
amini nina fursa kubwa zaidi ya kuwa mgombea.”
Akizungumzia idadi kubwa ya wana CCM wenzake
wanaojitokeza kuwania nafasi hiyo ya juu, alisema
hashangazwi hata kidogo kwani CCM ina hazina ya
viongozi wengi wenye sifa za urais japokuwa katika hao
waliojitokeza hakuna anayemuhofia.
“Tofauti na wale wenzetu, wao wana mtu mmoja mmoja
tu katika vyama vyao, ukizungumza CUF utamtaja
Lipumba na vyama vingine ni hivyo hivyo; ni sasa tu
baada ya kuunganisha vyama vyao kupitia umoja usio
rasmi angalau unaweza kuona kama wako wengi, lakini
kiuhalisia ni wale wale wanaotegemewa na vyama vyao,”
alisema.
Alisema hali hiyo ni tofauti na kabisa na CCM na
akawasihi wagombea wenzake wasipende
kuzunngumzia majina ya watu kama anavyofanya yeye.
“Katika harakati zangu zote sipendi kuzungumzia majina
ya watu, tunazungumza hoja, tunazungumza uchumi,
umasikini, ufisadi, rushwa na mengineyo kama hoja,
hatuzungumzi ufisadi kwa kulenga watu,” alisema.
Alisema katika kinyang’anyiro hicho anayelenga watu
atakuwa anahukumu watu huku vitabu vitakatifu
vikiwakataza kuwahukumu wengine ili nao
wasijehukumiwa.
“Habari ya ufisadi na mafisadi ni msamiati ulioingizwa
na wapinzani wetu. Mimi kama Wasira sina majina ya
watu mfukoni mwangu ambao naweza kusema nikiingia
Ikulu nitawashughulikia,” alisema.
Alisema endapo atapata ridhaa hiyo, ufisadi na rushwa,
atavishughulikia kama hoja kwa ahadi ya kutovifumbia
macho kwasababu vyote vinaua nchi na kuwafanya watu
waone haki sio haki.
“Katika kipindi hiki wana CCM lazima kazi yetu iwe ni
kuwaelimisha wananchi wakijue chama chetu na kujenga
umoja. Hatutakiwa kuzozana wenyewe kwa wenye, hiyo
itatupunguzia nguvu badala ya kutuimarisha, kumbukeni
Iringa mlivyohitilafiana mwaka 2010 na kupoteza jimbo
la Iringa Mjini kwa wapinzani,” alisema.
Alisema katika utawala wake atatilia mkazo kilimo cha
kisasa kwa kutumia zana za kisasa na kujenga viwanda
vya kisasa ili mazao yaweze kuongezewa thamani.

No comments:

Post a Comment