Friday, June 17, 2016

WAFANYAKAZI WA HOTELI YA SOUTHERN SUN WAFANYA USAFI KWENYE FUKWE ZA BAHARI YA HINDI


WAFANYAKAZI  wa Hoteli ya Southern Sun ya jijini Dar es Salaam leo wameadhimisha Siku ya Usafi wa Fukwe za Bahari Duniani kwa kufanya usafi wa kwenye fukwe za maeneo ya Salender Bridge jijini Dar es Salaam.
 
Wafanyakazi hao wamesema wamechukua hatua hiyo ili kuthamini siku hiyo inayoadhimishwa duniani kote na kuionesha dunia kwamba Tanzania ni moja ya nchi zinazojali hatua hiyo ya kuziweka fukwe za bahari katika hali ya usafi kwa ajili ya kuviokoa viumbe mbalimbali vinavyoishi baharini.
Aidha akizungumza na Blog ya Bayana Mratibu wa shughuli hiyo, Halima Nneka, alisema kuwa hiyo wao imekuwa ni tabia yao ya kufanya usafi kwenye sehemu mbalimbali za fukwe za bahari kwa kuwa wanathamini sana mazingira hayo kuwa katika hali ya usafi kwani inasaidia hata vijana na watu wanaotembelea maeneo hayo kujali na kuiga mfano wao huo.
“Kwakweli huwezi ukaenda pahala ambako ni safi, halafu wewe uitumie sehemu hiyo na kisha  uiwache ikiwa katika hali ya uchafu. Kwa mtu mstaarabu lazima naye atafanya usafi katika sehemu hiyo, aliyoikuta ikiwa safi kabla ya kuitumia,”alisema Mneka.
Aidha amezitaka Taasisi mbalimbali jijini Dar es Salaam, zilizoko kwenye maeneo ya Bahari kutenga walau hata siku moja katika mwezi kwa ajili ya kufanya usafi wa mazingira kwenye sehemu za fukwe za bahari, kwani ni sehemu ambazo jamii na wageni mbalimbali wanaoingia nchini hupenda kutembelea kwa ajili ya kupumzika na kupata hewa safi.
Wafanyakazi wa Hoteli ya Southern Sun ya jijini Dar es Salaam wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya kuanza kufanya usafi kwenye fukwe za maeneo ya Salender Bridge jijini Dar es Salaam, katika kuadhimisha Siku ya Usafi wa Fukwe za Bahari Duniani leo. 

No comments:

Post a Comment