Sunday, February 21, 2016

Wanafunzi 2,000 wasomea chini ya miti......

Wanafunzi 2,000 wasomea chini ya miti


Wanafunzi wakiwa darasani wakijisomea chini ya
Wanafunzi wakiwa darasani wakijisomea chini ya mti.Picha ya Maktaba. 
By Shaaban Ndyamukama, Mwananchi mwananchipapers@mwananchi.co.tz
Biharamulo. Wanafunzi 2,100 wa chekechea na darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Nyakanazi wilayani Biharamulo, wanalazimika kusomea chini ya miti kutokana na upungufu wa vyumba vya madarasa.
Kutokana na changamoto hiyo walimu wameiomba Serikali kwa kushirikiana na wazazi kuwajengea vyumba vya madarasa ili kuondokana adha wanayoipata.
Maombi hayo yalitolewa juzi baada ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongela kutembelea shule hizo akiambatana na maofisa wa halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo kubaini utekelezaji wa agizo la Serikali la kuandikisha wanafunzi wa awali na darasa la kwanza baada ya kutangazwa utoaji wa elimu bure.
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Nyakanazi, Janepha Francis alisema shule hiyo ina wanafunzi 4,200 jambo linalosababisha mrundikano katika madarasa.
Ofisa Elimu Msingi Wilaya ya Biharamulo, Rumanywa Mutashobya alisema halmashauri hiyo kwa kushirikiana na wananchi imeanzisha ujenzi wa shule mbili katika vitongoji vya Kabale na Nyakafundikwa.
Alisema wanafunzi zaidi ya 1,300 wa darasa la kwanza na awali wanatoka katika vitongoji hivyo.
Mongela alimwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo, Nassib Mbaga kuhakikisha ifikapo Machi Mosi mwaka huu, vyumba viwili vya madarasa vijengwe katika Shule ya Nyakanazi.

No comments:

Post a Comment